Nafasi Ya Matangazo

April 24, 2024

Mkurugenzi wa Miradi – Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Bw. John Steven.

Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika kipindi cha awamu ya pili ya utekelezaji iliyoanza mwaka 2020 umefanikiwa kutoa ruzuku ya zaidi ya shilingi bilioni 800 Tanzania bara na visiwani na kufanikiwa kuimarisha kiuchumi wa kaya maskini katika kuhakikisha wanapiga hatua katika maendeleo.

Akizungumza leo Aprili 24, 2024 katika Maonesho ya Maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano yanayofanyika kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Miradi – Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Bw. John Steven, amesema kuwa walengwa wamefanikiwa kuimarika kiuchumi na kuweza kusaidia familia zao ikiwemo kusomesha na kujenga nyumba.

Bw. Steven amesema kuwa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa sasa wametoa ruzuku shilingi bilioni 17.5 kwa halmashauri mbalimbali Tanzania Bara na Visiwani katika maeneo ya utekelezaji 35, huku maeneo 18 yakiwa katika mchakato wa utekelezaji.

“Miongoni mwa majukumu yetu ni kuunda vikundi ili wanachana waweze kujitegemea, pia kutoa ruzuku ya uzalishaji ambapo ni eneo jipya; TASAF imeanza kutekeleza kwa awamu ya pili ya Mpango Kunusuru Kaya za Walengwa“, amesema Bw. Steven.

Amefafanua kuwa wanachama wanaofanya vizuri katika vikundi wanapewa fedha wastani wa shilingi 350,000 kwa ajili ya kuongeza mtaji katika biashara ambazo tayari wameanza kufanya“, amesema Bw. Steven.

Amesema kuwa kazi yao ni kuinua kaya maskini na wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa kama inavyoonekana katika maonesho ambapo vikundi mbalimbali kutoka bara na visiwani wameshiriki kuonesha shughuli zao za kilimo pamoja na biashara.

Bw. Steven amesema kuwa TASAF ni mpango unaotekelezwa Tanzania bara na Visiwani na sasa wapo katika awamu ya pili ya utekelezaji wa Kunusuru Zaya za Walengwa.

Amesema kuwa wapo katika maeneo ya utekelezaji 186 ambazo ni halmashauri zote za Tanzania bara na visiwani ikiwa na kazi kubwa ya kutoa ruzuku pamoja na kutoa ajira za muda, kuimarisha miundombinu, idara mbalimbali wanazoshirikiana nazo pamoja na kukuza uchumi wa kaya kupitia vikundi vya kuweka na kukopeshana.

Ameeleza kuwa Tanzania bara na visiwani kuna vikundi 56,000 kati ya hivyo vikundi 49,000 sawa na asilimia 88 tayari vimeingizwa katika mfumo, huku vingine vikiwa katika utaratibu wa kuingizwa katika mfumo huo.

Amesema kuawa vikundi 49,000 ambavyo vipo katika mfumo vinatoa fursa ya muda wowote kuweza kupata taarifa zao za utendaji.

Bw. Steven amesema kuwa kupitia vikundi 56,000 mpaka sasa kuna wanachama 778,000 kati ya hao wanaume ni 115,000 huku wanawake wakiwa 663,000.

TASAF inashirikia katika Maonesho ya Maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano yanayofanyika kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam yakiwa na kauli mbiu : Tumeshikamana, tumeimarika kwa maendeleo ya Taifa.

 

Posted by MROKI On Wednesday, April 24, 2024 No comments
 
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa katika mwaka 2024/25 Serikali itaendelea kutekeleza hatua madhubuti za kuimarisha matumizi ya Nishati Safi ya kupikia nchini.

Amesema hayo leo Aprili 24, 2024 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka 2024/25

“Serikali kwa kushirikiana na wadau itaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024 – 2034 kwa kupatia ufumbuzi vikwazo vya matumizi ya nishati hiyo, ikiwemo gharama kubwa, upatikanaji hafifu na uhaba wa miundombinu yake na kukosekana kwa elimu ya kutosha kuhusu madhara ya nishati zisizo safi na salama za kupikia”, amesema Dkt. Biteko.

Ameongeza “Wizara itaendelea kusimamia na kuratibu utekelezaji wa Programu ya Nishati Safi ya Kupikia inayolenga Kuwawezesha Wanawake Barani Afrika Kutumia Nishati Safi ya Kupikia”.

Pia, Dkt. Biteko amebainisha kuwa Serikali pia itaendelea na utekelezaji wa mradi wa kusambaza majiko banifu kwenye kaya zilizopo katika maeneo ya vijijini na vijiji-miji, kutoa ruzuku kwa wazalishaji wa mkaa mbadala kwa ajili ya ununuzi wa mashine zitakazotumika katika uzalishaji wa mkaa huo, kuendelea kushirikiana na Jeshi la Magereza katika ujenzi wa miundombinu ya nishati ya kupkia katika maeneo 211 pamoja na kuendelea na usambazaji wa gesi asilia majumbani, hususan katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi na Pwani. 

Wizara ya Nishati imewasilisha maombi ya shilingi 1,883,759,455,000 kwa ajili ya matumizi ya Wizara hiyo na Taasisi zake.
Posted by MROKI On Wednesday, April 24, 2024 No comments
Serikali imesema hadi kufikia Mwezi, Machi 2024 jumla ya vijiji 11,837 sawa na asilimia 96.37 ya vijiji vyote 12,318 vya Tanzania Bara vilikuwa vimeunganishiwa huduma ya umeme. 

Hayo yamesema na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko Bungeni, leo Tarehe 24 Aprili, 2024, Jijini Dodoma wakati akisoma Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa mwaka 2024/2025. 

Aidha, Dkt. Biteko amesema katika kuimarisha utoaji wa huduma kwa Wananchi vijijini, jumla ya taasisi 63,509 zinazotoa huduma kwa jamii ikiwemo ya elimu, biashara, pampu za maji, vituo vya afya na nyumba za ibada zilikuwa zimeunganishiwa umeme, ikilinganishwa na taasisi 43,925 Mwezi Aprili, 2023.

Vilevile, Serikali imeendelea kuchukua hatua za kupeleka umeme vitongojini na katika visiwa na maeneo yaliyo mbali na Gridi ya Taifa, vituo vya afya na pampu za maji, wachimbaji wadogo wa madini, viwanda na kilimo, katika shule pamoja na mahakama za mwanzo vijijini.

Dkt. Biteko amesema katika mwaka 2024/25, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) itaendelea kupeleka nishati vijijini ili kuchochea kasi ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii katika maeneo hayo. Miradi iliyopangwa kutekelezwa ni pamoja mradi wa kupeleka umeme katika Vitongoji 20,000 ambapo kazi zitakazofanyika ni pamoja na ununuzi wa wakandarasi wa kutekeleza mradi, kufanya usanifu wa kina wa mradi na kuanza ujenzi wa miundombinu ya mradi.

Miradi mingine ambayo itapewa kipaumbele ni pamoja na Mradi wa kupeleka umeme katika Vitongoji 3,060 (vitongoji 15 kila Jimbo) kwa kujenga miundombinu ya mradi, kufunga transfoma na kuunganisha wateja.

Miradi mingine, itakayotekelezwa ni mradi wa Ujazilizi Awamu ya Pili (B); Mradi wa Ujazilizi Awamu ya Pili (C); Mradi wa kupeleka umeme katika maeneo ya Vijijini-Miji; (PERI Urban); Mradi wa kusambaza umeme katika Migodi Midogo, Maeneo ya Kilimo na Viwanda; Mradi wa kupeleka umeme katika minara ya mawasiliano ya simu na mradi wa ufungaji wa mifumo ya umeme jua kwenye makazi yaliyopo Visiwani na yaliyopo mbali na Gridi ya Taifa.  

Kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, Dkt. Biteko amesema Serikali kwa kushirikiana na Wadau, itaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024 – 2034 kwa kupatia ufumbuzi vikwazo vya matumizi ya nishati hiyo, ikiwemo gharama kubwa, upatikanaji hafifu na uhaba wa miundombinu yake na kukosekana kwa elimu ya kutosha kuhusu madhara ya nishati zisizo safi na salama za kupikia.

Aidha, Mradi wa kusambaza majiko banifu kwenye Kaya zilizopo katika maeneo ya Vijijini na Vijiji-Miji; kutoa ruzuku kwa wazalishaji wa mkaa mbadala kwa ajili ya ununuzi wa mashine zitakazotumika katika uzalishaji wa mkaa huo; kuendelea kushirikiana na Jeshi la Magereza katika ujenzi wa miundombinu ya nishati ya kupikia katika maeneo 211 pamoja na kuendelea na usambazaji wa gesi asilia majumbani, hususan katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi na Pwani.  
Posted by MROKI On Wednesday, April 24, 2024 No comments




Waziri wa Madini, Mhe Anthony Mavunde amebainisha kwamba Serikali kupitia Tume ya Madini imefuta jumla ya maombi ya leseni 227 ambayo yamekosa vigezo vya kuendelea kufanyiwa kazi.

Ameyasema hayo leo tarehe 24 Aprili, 2024 Jijini Dodoma alipokuwa akizungumza katika mkutano na vyombo vya habari.

"Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wetu mpendwa Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka kipaumbele katika kuendeleza sekta ya madini nchini. Ndugu zangu nataka niwaambie kwamba sisi Wizara ya Madini hatupo tayari kufifisha juhudi hizi njema za kiongozi wetu."

"Na ndiyo maana mwezi uliopita tulitangaza kufuta jumla ya maombi na leseni 2,648. Wengi walidhani sisi tunafanya utani, nataka niwaambie Serikali hatupo tayari kuona watu wachache wanashikilia maeneo pasipo kuyaendeleza kwa mujibu wa Sheria ya Madini, Sura ya 123." Alieleza Mhe. Mavunde.

Pia, Mhe Mavunde alibainisha kwamba maombi hayo 227 yamefutwa kutokana na sababu ya kutolipiwa ada stahiki za maombi kwa mujibu wa Sheria pamoja na kukosa nyaraka zinazotakiwa kuambatishwa na maombi hayo.

Aidha, Mhe. Mavunde alieleza kwamba uchambuzi uliofanywa na Tume ya Madini umebaini kuwa kuna watumiaji wa mfumo wa uwasilishaji maombi kwa njia ya mtandao wapatao 34 wanatumia mfumo vibaya kwa kuwasilisha maombi bila kulipa Ada stahiki.

Vilevile, Mhe. Mavunde alisisitiza kuwa Wizara ya Madini itaendelea kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais ya kuhakikisha sekta ya madini inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika uchumi wa Nchi yetu, na hivyo wale wote ambao hawapo tayari kufuata Sheria na taratibu za madini zilizopo hatafumbiwa macho.

Katika hatua nyingine, Mhe. Mavunde alieleza kwamba tangu alipotangaza kufuta leseni 2,648 mnamo tarehe 22 Machi, 2024  kumekuwepo na umakini mkubwa wa uwasilishaji wa maombi na kufanyika kwa malipo kwa mujibu wa sheria ambapo jumla ya mapato ya shilingi 2,430,647,335.99 yamekusanywa na Tume ya Madini, fedha hizo zimetokana na waombaji na wamiliki wengi wa leseni kuzingatia na kufuata taratibu za kulipia leseni na maombi yao kwa mujibu wa Sheria.

Akihitimisha taarifa yake, Mhe. Mavunde aliielekeza Tume ya Madini kuendelea na uchambuzi wa leseni na maombi ili kuendelea kubaini maombi na leseni ambayo hayakidhi vigezo vya kisheria kwa ajili ya kuendelea kufuta kupisha waombaji wengine wenye uhitaji wa kuendeleza maeneo hayo.
Posted by MROKI On Wednesday, April 24, 2024 No comments
 




Na Eleuteri Mangi, Arusha
Waendesha baiskeli wa timu ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi wameibuka mabingwa wa mchezo wa kuendesha baiskeli kwa wanaume na wanawake katika Michuano ya Michezo ya Mei Mosi 2024 inayoendelea kupamba moto jijini Arusha.

Kwa wanaume ambao wameendesha baiskeli kwa KM 55, James Shigela ametumia muda wa saa 1:27 na Alavuya Michael Ntalima kwa wanawake ambao waliendesha baiskeli kwa umbali wa KM 35 ametumia saa 1:05.

Nafasi ya pili kwa wanaume imekwenda kwa Hassan Ligoneko kutoka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambaye alitumia saa 1:30, nafasi ya tatu imekwenda kwa Stevine Sanga kutoka Hospitali ya Ocean Road ambaye ametumia saa1:30:14 wakati kwa upande wa nafasi ya pili kwa wanawake imekwenda kwa Scholastica Asili kutoka Wizara ya Uchukuzi ambaye ametumia saa 1:05:25 na nafasi ya tatu imechukuliwa na Ester Chacha kutoka Wizara ya Afya ambaye ametumia saa 1:28.

Michezo hiyo mefikia hatua ya robo fainali ambayo ni mpira wa miguu, netiboli, kamba wanaume na wanawake pamoja na mpira wa wavu wannaume na wanawake.

Baadhi ya timu zilizofuzu hatua hiyo katika mpira wa miguu ni Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ambao waliwafunga Wizara ya Fedha magoli 5:0, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi wamewafunga timu ya Wizara ya Afya magoli 2-0, timu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wameifunga timu ya Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora magoli 2-0 na timu ya TANROADS wamewafunga Meru DC 3-1.

Katika mchezo wa Netiboli, timu ya Ofisi ya Rais TAMISEMI wamewafunga timu ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) jumla ya magoli 103-0, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa wamewafunga Shirikanla Viwango Tanzania (TBS) magoli 69-7, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi wameibuka kidedea kwa kuwafunga NSSF kwa magoli 30-20, Ofisi ya Rais Ikulu wamewafunga Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora magoli 37-20.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Aprili 30, 2024 yakifuatiwa na maadhidhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani Mei Mosi ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa ni Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Posted by MROKI On Wednesday, April 24, 2024 No comments

April 23, 2024

Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete akishiriki katika maandamano ya amani kuelekea uzinduzi wa Jukwaa la kuwawezesha wanawake kiuchumi Kata ya Kiwangwa, Tarafa ya Msata. 
Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete akishiriki katika maandamano ya amani kuelekea uzinduzi wa Jukwaa la kuwawezesha wanawake kiuchumi Kata ya Kiwangwa, Tarafa ya Msata.
Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete akizungumza wakati wa 25 uzinduzi wa Jukwaa la kuwawezesha wanawake kiuchumi Kata ya Kiwangwa, Tarafa ya Msata
Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amezindua Jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi Kata ya Kiwangwa, Tarafa ya Msata. 

Sherehe hizo zilizopambwa na maandamano ya Amani yakifuatiwa na mjadala kuhusu uwezeshaji na fursa mbalimbali za kumkomboa na kumuwezesha Mwanamke katika jamii.

Kikwete alisema kupitia fursa mbalimbali zilizopo zikiwemo za ndani ya Halmashauri na zile zinazo simamiwa na Serikali kuu wanawake wana nafasi ya kusaidia ukuaji wa kipato ndani ya jamii na familia.

 "Kwa mujibu wa Taarifa za Sensa, ongezeko wa idadi ya Wanawake wanaotegemewa ndani ya Familia umeongezeka  kufikia asilimia 37.6. Idadi hii inatoa fursa za kuwezesha wanawake katika jamii," alisema Kikwete.  

Aidha alisema Serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali ikiwemo kurudisha mikopo ya asilimia 10, mfuko kusaidia Wananchi kuendelea kutenga fedha kuwezesha wananchi kiuchumi na fursa nyenginezo. 

Kikwete ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze aliwaunga mkono kupitia ofisi ya Mbunge ambayo ilichangia Shilingi Milioni 4.6 kuwezesha vikundi kukopeshana.
Posted by MROKI On Tuesday, April 23, 2024 No comments
 




Naibu Waziri wa Utumishi na Utawala Bora Ndg. Ridhiwani Kikwete amewataka WAHITIMU wa kidato cha sita katika shule ya Kati ya Lugoba , Halmashauri ya Chalinze  Mkoani Pwani kufanya vizuri katika mitihani yao.

Kikwete ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze ameyasema hayo wakati  akihutubia wahitimu wa kidato cha Sita katika mahafali shuleni hapo leo.

Kikwete aliwaasa wahitimu hao kuhakikisha wanafaulu ili waache deni la kufuatwa na wadogo zao wanaowafuata kwa upande mmoja, wawape heshima Walimu na wazazi pia kwa kufaulu vizuri.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha Mbunge kuzungumza na Wahitimu, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Sakasa aliishukuru serikali kwa kuendelea kupeleka pesa za Elimu bure , vifaa na kuongezeka kwa madarasa na walimu shuleni hapo huku akimuomba Mgeni rasmi kuendelea kuikumbuka shule hiyo kwa kuisaidia vifaa na kuongeza mabweni ya wanafunzi. 
Posted by MROKI On Tuesday, April 23, 2024 No comments
Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego akishiriki zoezi la usafi katika Soko Kuu la Mji wa Singida akiwa na Wananchi wa Singida.
Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego akizungumza na Wakazi wa Mji wa Singida mara baada ya kumaliza shughuli za usafi katika Soko Kuu la Singida ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Mkuu wa wilaya ya Singida Godwin Gondwe  akifanya usafi na wananchi katika soko kuu la Singida.
Mkuu wa wilaya ya Singida Godwin Gondwe akizungumza na wakazi wa mji wa Singida kabla ya kumkaribisha Mkuu wa mkoa Kuzungumza na Wakazi wa Mji wa Singida walioshiriki zoezi la Usafi.


Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego akishiriki zoezi la usafi katika Soko Kuu la Mji wa Singida akiwa na Wananchi wa Singida.

Mkuu wa mkoa wa Singida Halima Dendego ameonya kuwa atawachukulia hatua kali watu au kikundi cha watu wanaotaka kuvuruga au kuvunja amani na utulivu kwa wananchi wa mkoa wa Singida.

Mkuu wa mkoa wa Singida ametoa kauli hiyo (leo 23/Apr/24 ) mjini Singida, katika uzinduzi wa wiki ya maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa kufanya usafi katika maeneo mbalimbali ya Soko Kuu la Singida.

Mkuu huyo wa mkoa wa Singida amewasisitiza wananchi wa mkoa wa Singida kuwakataa watu au mtu yeyote anayetaka kumdhalilisha Rais au Watanzania kwani wakiwaruhusu kufanya hivyo watakuwa wamedhalilisha Taifa na Watanzania wote hivyo ni lazima wananchi wote waungane kukataa watu hao wenye nia mbaya na Taifa la Tanzania.

“Tuungane wote katika kupambana na yeyote anayetaka kuleta ujinga ujinga katika Taifa letu tuwabaini ili tuwawajibishe “ Amesisitiza Halima Dendego.

Halima Dendego amesema yeye ni rafiki wa wote Vijana,Wazee na Wanawake hivyo Ofisi yake ipo wazi muda wote kwa anayetaka kusaidiwa kwa shida yeyote aende ili asaidiwe nia ni kuona wananchi Singida wanaishi maisha mazuri na yenye staha bila kero. 

Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Singida Godwin Gondwe amemhakikishia Mkuu wa mkoa wa Singida kuwa atasimamia maelekezo yake yote aliyotoa hasa ya kuhakikisha Manispaa ya Singida inakuwa safi katika maeneo yote ya Masoko na maeneo yenye watu wengi kama hatua ya kudhibiti magonjwa ya maambukizi ikiwemo kipindupindu.

Godwin Gondwe amesema kuwa hivi karibuni watazindua kampeni kubwa ya usafi katika Manispaa ya Singida ambayo itasaidia kuboresha usafi katika maeneo yote ya mji wa Singida ikilinganishwa na hali ilivyo sasa.

Naye, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida Edward Mboya amebainisha kuwa kupitia mapato ya ndani wanaendelea na mchakato wa kununua gari nyingine mpya ya kubebea taka na vifaa vya kuhifadhi taka lengo ikiwa ni kuifanya Manispaa ya Singida kuwa bora nchini hasa katika masuala ya Usafi.


 Mkuu wa wilaya ya Singida Godwin Gondwe akizungumza na wakazi wa mji wa Singida kabla ya kumkaribisha Mkuu wa mkoa Kuzungumza na Wakazi wa Mji wa Singida walioshiriki zoezi la Usafi.
Posted by MROKI On Tuesday, April 23, 2024 No comments

April 22, 2024







Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde leo Aprili 22, 2024 jijini Dodoma amekutana na wafanyabiashara wa madini na wachimbaji wa madini kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili kwenye shughuli zao ikiwemo changamoto ya ukosekanaji wa teknolojia ya uchenjuaji wa baadhi ya madini na hivyo kuielekeza Tume kuandaa utaratibu sahihi wa usafirishaji wa madini yaliyongezwa thamani kwa kiwango cha teknolojia inayopatikana hapa nchini.

Ametoa maelekezo hayo, mara baada ya kusikiliza changamoto za wafanyabiashara wa madini na wachimbaji wa madini ikiwemo zuio la kusafirisha madini ghafi lililotolewa na Serikali mapema mwaka 2017 ambapo wameomba Serikali kuwapa muda wa kusafirisha madini yaliyoongezwa thamani kwa kiwango cha teknolojia inayopatikana nchini kwa sasa kutokana na kutokuwepo kwa viwanda vya kuchenjua madini hayo hali iliyowasababishia kuendesha shughuli zao kwa hasara.

“Naielekeza Tume ya Madini kuweka utaratibu maalum wa usafirishaji wa madini hayo kwa kipindi cha mpito cha mwaka mmoja wakati mkijipanga kuhakikisha madini yanachenjuliwa ndani ya nchi kwa kiwango kikubwa” amesema Mavunde.

Amesema kuwa, lengo la Serikali la kuweka mkazo wa kuyaongezea thamani madini yote nchini ni kuongeza faida kwa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini huku Serikali ikipata kodi zaidi, hivyo Sekta ya Madini kuendelea kuwa na mchango kwenye Pato la Taifa.

Aidha, amewataka wadau wa madini kuwekeza kwenye viwanda vya uchenjuaji wa madini sambamba na kuwakaribisha wawekezaji kutoka nje ya nchi kwenye ujenzi wa viwanda  hivyo na kuongeza kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini ipo tayari kutoa ushirikiano kwa wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye viwanda vya kuchenjua madini nchini.

“Muda wote milango ya ofisi yangu ipo wazi kwa mwekezaji yeyote mwenye nia ya kuwekeza kwenye kiwanda cha kuongeza thamani  madini nchini, tunataka kuhakikisha Serikali inapata kodi zaidi fedha ambazo zinatumika kwenye uboreshaji wa  huduma za jamii kama vile barabara, maji, vituo vya afya sambamba na kufungua fursa za ajira huku wadau wa madini wakiendelea kutajirika,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Katika hatua nyingine amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Madini itaendelea kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji nchini ikiwa ni pamoja na sheria na kanuni bora za madini, miongozo mbalimbali, kodi na tozo rafiki ili kuvutia wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi.

Ameongeza mikakati mingine kuwa ni pamoja na kuendelea kufanya tafiti mbalimbali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) na uanzishaji wa maabara ya kisasa ili kuhakikisha wachimbaji wa madini wanaendesha shughuli zao kwa uhakika na kutajirika.

“Kama Wizara ya Madini kupitia Vision 2030 ya Madini ni Maisha na Utajiri tumeweka lengo la kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 utafiti wa kina wa madini nchini (high resolution) uwe umefikia asilimia 50 kutoka asilimia 16 ya sasa; mpaka sasa tumeshafanya tafiti katika maeneo ya Dodoma, Geita, Kahama, Mirerani, Lindi na Mtwara,” amesema Mavunde.

Awali akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Kheri Mahimbali amesema kuwa lengo la kikao hicho lilikuwa ni kusikiliza kero za wafanyabiashara na wachimbaji wa madini na kuzitatua sambamba na kutoa ufafanuzi katika maeneo mbalimbali yahusiyo Sekta ya Madini.

Kikao hicho pia kimehudhuriwa na Kamishna wa Madini Nchini, Dkt. Abdulrahman Mwanga, Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba na menejimenti na watumishi kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini.
Posted by MROKI On Monday, April 22, 2024 No comments



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali itaajiri walimu wapya wa masomo ya sayansi na itaendelea kuboresha maslahi yao.

Rais Dk.Mwinyi amesema hayo alipofungua Skuli ya ghorofa ya Sekondari Hassan Khamis Hafidh iliopo Monduli, Wilaya ya Magharibi A , Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe 22 Aprili 2024 ikiwa ni shamrashamra za Miaka ya 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. 

Aidha Rais Dk.Mwinyi amewapongeza Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri ya kuvuka malengo ya ilani ya utekelezaji ya uchaguzi ya CCM 2020-2025.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi ameeleza kuwa ujenzi wa  miundombinu ya Skuli ina lengo la kuboresha ili kupunguza msongamano wa wanafunzi na kutozidi idadi ya 45 kila darasa.

Kwa upande mwingine Rais Dk.Mwinyi amewataka wananchi kuendelea kuudumisha Muungano ili kupata maendeleo katika nyanja zote.
Posted by MROKI On Monday, April 22, 2024 No comments







Na John Mapepele
Serikali imesema Tanzania inaongoza kwa kuwa na Simba, Nyati na Chui wengi katika bara la Afrika huku ikishirikilia nafasi ya tatu kwa kuwa na idadi kubwa yaTembo.

Hayo yamesemwa leo Aprili 22, 2024 kwenye mkutano ambao Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki ametangaza rasmi matokeo ya Sensa ya Wanyamapori na kuzindua taarifa ya Watalii wa Kimataifa walioitembelea Tanzania mwaka 2023.

Sensa hiyo ya wanyamapori imefanywa na TAWIRI kwa kushirikiana na TANAPA, TAWA, NCAA, Idara ya Wanyamapori, na Frankfurt Zoological Society katika mifumo ya ikolojia ya Nyerere-Selous-Mikumi,Saadani-Wamimbiki na Serengeti 

Mkutano huo uliwahusisha wadau wa uhifadhi na utalii, ambapo Mhe. Kairuki amesema tayari Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kufanya sensa ya wanyamapori nchi nzima mapema hapo mwakani.

 Aidha, Mhe. Kairuki amesema matokeo ya sensa hiyo yatasaidia kwenye usimamizi wa wanyamapori nchini na kupanga mipango mbalimbali ya kuboresha  uhifadhi na  kutangaza  utalii duniani.

Mhe. Kairuki ametoa wito kwa wadau wote kushirikiana na Serikali ambapo ameitaka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori nchini (TAWIRI) kuandaa mpango kazi kwa ajili ya sensa ijayo huku pia akielekeza watendaji wa wizara yake kuchambua kwa kina  matokeo ya sensa hii  ili yaweze kuleta tija.

Akitoa taarifa ya sensa hiyo amesema spishi zilizoonyesha idadi kubwa ni pamoja na Nyati (59,878), Tembo (20,006), Nyumbu (19,060), Kongoni (18,361), swalapala (14,031) na Ngiri (13,806), ambapo spishi zilizoonyesha idadi ndogo ni pamoja na Twiga (1,679), Tandala mkubwa/ kudu (1,414) na puku/sheshe (496). 

Amefafanua kuwa kwa upande wa Tembo, idadi imeongezeka kutoka 15,501 (2018) hadi 20,006 (2022) na Viashiria vya ujangili wa tembo au vifo vya tembo vimepungua kwa kiasi kikubwa hadi 0.8% mwaka 2022 ikilinganishwa na 16% wakati wa sensa ya 2018. 

Akizungumzia kuhusu taarifa ya Watalii wa Kimataifa walioitembelea Tanzania mwaka 2023 amesema Sekta ya Utalii ni miongoni mwa sekta muhimu katika uchumi wa dunia na umeendelea kuimarika baada kuathiriwa na mlipuko wa janga la UVIKO-19. Mwaka 2023 sekta ya utalii duniani imeimarika kwa kiwango cha asilimia 88 ikilinganishwa na kiwango cha juu kilichofikiwa mwaka 2019.

 “Hali hii ilitokana na ukuaji endelevu wa maendeleo ya teknolojia na juhudi za kukuza na kuendeleza maeneo mengine ya utalii duniani. Takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya watalii duniani iliongezeka kwa asilimia 34 hadi kufikia watalii bilioni 1.3 Mwaka 2023 kutoka milioni 960 Mwaka 2022”. Ameongeza

Amesema kwa Tanzania, utalii wa Kimataifa umeimarika kwa kiwango cha asilimia 118.4 Mwaka 2023 ikilinganishwa na kiwango cha juu kabla ya janga la UVIKO-19.  Aidha, idadi ya watalii wa Kimataifa iliongezeka kutoka watalii milioni 1.4 Mwaka 2022 hadi kufikia watalii milioni 1.8 Mwaka 2023 sawa na ongezeko la asilimia 24.3. 

“Hatuna budi kutambua kazi kubwa aliyoifanya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyeitangaza Tanzania kupitia filamu ya Tanzania the Royal tour”. Amesisitiza  


Kwa kutambua umuhimu wa sekta ya utalii hapa Nchini, Serikali kwa kushirikiana na wadau ilifanya utafiti wa watalii wanaoondoka Nchini Mwaka 2023 kwa lengo la kupata taarifa zinazosaidia kutunga Sera na kuandaa mipango ya maendeleo ya utalii. Aidha, taarifa za utafiti huo zinasaidia serikali kuandaa akaunti za taifa (national accounts) na mizania ya malipo ya nje (Balance of Payments). 

Aidha amesema utafiti umebainisha kuwa mapato yatokanayo na utalii yaliongezeka kwa asilimia 33.5 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 3.4 Mwaka 2023 kutoka Dola za Marekani 2.5 bilioni zilizopatikana Mwaka 2022.  Aidha, wastani wa matumizi ya mtalii kwa siku katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uliongezeka hadi kufikia Dola za Marekani 250 Mwaka 2023 kutoka wastani wa Dola za Marekani 214 Mwaka 2022. 

Kwa upande wa Zanzibar, wastani wa matumizi ya mtalii kwa siku ulikuwa Dola za Marekani 257 Mwaka 2023 ikilinganishwa na watani wa Dola za Marekani 218 Mwaka 2022.
Posted by MROKI On Monday, April 22, 2024 No comments
  • Facebook
  • Twitter
  • Youtube

Labels

Blog Archive

Nafasi Ya Matangazo